Saturday, October 31, 2015

Hizi ndizo faida 50 za mazoezi

Moja ya mahitaji matano (5) mhimu ili kuishi baada ya oksijeni, majichumvi, na potasiamu; ni Mazoezi. Mazoezi ni mhimu kwa ajili ya afya zaidi ya kuwa na maumbile ya kuvutia (sex body), burudani au kitu kingine chochote.
Watu wengi hufuatilia kuhusu chakula tu, hata kama utakula vizuri vipi bila mazoezi mlo haujakamilika, kwa hiyo mazoezi ni mhimu kwa yeyote kama ilivyo kwa maji au chakula.

Hizi ndizo faida 50 za mazoezi

Zifuatazo ni moja ya sababu 50 mhimu za kufanya mazoezi kwa afya bora na maisha marefu bila maumivu:
1. Hukufanya ujisikie vizuri
2. Huongeza uwezo wa kujifunza
3. Hujenga uwezo wa kujistahi
4. Huongeza nguvu ya ubongo kufanya kazi
5. Huuweka mwili wako kuwa unaofaa (fit) na wenye uwezo
6. Huongeza afya ya akili yako
7. Huongeza kinga ya mwili
8. Hupunguza mfadhaiko/stress
9. Hukufanya ujisikie vizuri/mwenye furaha
10. Hukufanya usizeeke mapema
11. Huweka ngozi yenye mng’aro na yenye afya
12. Husaidia kupata usingizi mtulivu
13. Husaidia kuzuia ugonjwa wa kiharusi/strokes
14. Huongeza ufanisi katika makutano/joints ya mwili
15. Huongeza nguvu za mishipa
16. Huondoa wasiwasi
17. Huongeza kumbukumbu
18. Husaidia kudhibiti ulevi/uteja
19. Huongeza uzarishaji
20. Huongeza uwezo wa ubunifu
21. Hupendezesha muonekano wa mwili
22. Huongeza uwezo wa kujiamini
23. Husaidia kuongeza nguvu juu ya malengo yako maishani
24. Huondoa tatizo la kukinaishwa na chakula
25. Huongeza miaka ya kuishi
26. Hukomaza mifupa
27. Huongeza afya ya moyo
28. Huongeza hali ya kuwa na msimamo
29. Huondoa homa ndogo ndogo mwilini
30. Huongeza hamu ya kula
31. Hudhibiti usawa wa lehemu/kolesteroli
32. Hupunguza uwezekano wa kupatwa na baadhi ya kansa
33. Hushusha shinikizo la juu la damu/BP
34. Hupunguza uwezekano wa kupatwa na kisukari
35. Huzuia kupatwa na ukichaa/uwendawazimu
36. Hupunguza au huzuia maumivu ya mgongo
37. Hupunguza uwezekano wa kupatwa na ugonjwa wa mifupa
38. Hupunguza hisia/fikra za kujisikia vibaya au huzuni
39. Huzuia kupotea kwa mishipa
40. Huongeza nguvu na ustahimilivu
41. Huongeza ufanisi katika michezo
42. Huongeza uwezo wa kuvumilia maumivu
43. Huongeza usawa na ushirikiano wa mwili
44. Huongeza usambazaji wa oksijeni katika seli za mwili
45. Huongeza hali ya ufuatiliaji/concentration
46. Huongeza uwezo wa kujitawala na kujidhibiti nafsi
47. Huondoa uchovu
48. Huongeza nguvu katika tendo la ndoa
49. Hufanya maisha ni yenye kuvutia zaidi
50. Huongeza ubora wa maisha
Mazoezi yafuatayo ni mazuri sababu ya thamani yake ya baadaye na hayasababishi maumivu kwenye maungio, nayo ni; kutembea kwa miguu, kuogelea, kuendesha baiskeli, kucheza tenisi, gofu, kukwea, kudansi na kadharika.
Share:

Kitunguu Swaumu hutibu magonjwa 30

MUNGU anaposema watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa hamaanishi maarifa ya kutengeneza au kuendesha ndege, ni maarifa ya kawaida tu katika maisha yetu ya kila siku ambayo yanaweza kubadilisha afya na ustawi wetu. Moja ya mmea ambao umependelewa sana na Mungu kwakuwa na viinilishe vingi na mhimu sana kwa afya ya binadamu ni kitunguu swaumu. Kitunguu swaumu ni dawa karibu kwa kila ugonjwa.
Huko sokoni tayari nimeviona vitunguu swaumu kutoka China na Afrika kusini ambavyo vyenyewe huwa vina punje kubwa nene na huwa rahisi kuvimenya, hata hivyo ili upate faida hizi zote hapa chini naendelea kukushauri utumie vitunguu swaumu vyetu vinavyolimwa hapa Tanzania kwani hivyo vya kutoka nje pamoja na kuwa ni rahisi kuvimenya lakini ubora wake si kama ule wa vitunguu vyetu.
Hakikisha kila mboga unayopika haikosi kitunguu swaumu ndani yake na ikibidi ukiweke mwishoni mwishoni unapokaribia kuipuwa mboga yako toka katika moto kwamba kisiive sana hata kupoteza viinilishe vyake. Kama una friza au friji ya kawaida unaweza kumenya vitunguu swaumu hata kilo nzima na kuvitwanga kidogo katika kinu, vifunge vizuri katika bakuli au mfuko wa plastiki na uvihifadhi katika friza au friji na hivyo kila unapopika unachukuwa tu na kukitumia ili kuepuka usumbufu wa kukimenya kila siku.
Lakini ili upate faida zaidi za kitunguu swaumu utatakiwa ukimeze katika majikikiwa kibichi, yaani bila kupitishwa katika moto au kuwa kimepikwa.
Chukuwa kitunguu swaumu kimoja
kitunguu swaumu
kitunguu swaumu

Kigawanyishe katika punje punje
kitunguu swaumu
kitunguu swaumu

Menya nusu yake (punje 8 au 10 hivi),
kitunguu swaumu
kitunguu swaumu

Menya punje moja baada ya nyingine
kitunguu swaumu
kitunguu swaumu

Kisha vikatekate (chop) vipande vidogo vidogo na kisu
kitunguu swaumu
kitunguu swaumu
Meza kama unavyomeza dawa na maji vikombe 2 kila unapoenda kulala au fanya kutwa mara 2 kama unaumwa na moja wapo ya magonjwa niliyoyaorodhesha hapa chini.
Fanya hivi kila siku au kila mara unapopata nafasi na hivyo utakuwa mbali na kuuguwauguwa. Mama mjamzito chini ya miezi 4 ni vema asitumie, kwa ujumla tu mjamzito uwe makini utakapotumia kitunguu swaumu kwa namna hii kama wewe ni mjamzito.
kitunguu swaumu
Kitunguu swaumu kilichokatwakatwa/chopped

Kitunguu swaumu hutibu magonjwa 30

Haya ni baadhi ya magonjwa yanayotibika au kukingika na kitunguu swaumu:
  1. Huondoa sumu mwilini
  2. Husafisha tumbo
  3. Huyeyusha mafuta mwilini (kolestro)
  4. Husafisha njia ya mkojo
  5. Hutibu amoeba, minyoo na Bakteria
  6. Huzuia kuhara damu (Dysentery)
  7. Huondoa Gesi tumboni
  8. Hutibu msokoto wa tumbo
  9. Hutibu Typhoid
  10. Huondoa mabaka mabaka kwenye ngozi
  11. Hutibu mafua na malaria
  12. Hutibu kifua kikuu
  13. Hutibu kipindupindu
  14. Hutibu upele
  15. Huvunjavunja mawe katika figo
  16. Hutibu mba kichwani
  17. Huupa nguvu ubongo
  18. Huzuia meno kung’ooka na kutuliza maumivu
  19. Huongeza SANA nguvu za kiume
  20. Hutibu maumivu ya kichwa
  21. Hutibu kizunguzungu
  22. Hutibu shinikizo la juu la damu
  23. Huzuia saratani/kansa
  24. Hutibu maumivu ya jongo/gout
  25. Huuongezea nguvu mfumo wa mmeng’enyo wa chakula
  26. Huongeza hamu ya kula
  27. Huzuia damu kuganda
  28. Husaidia kutibu kisukari
  29. Husaidia kutibu tatizo la kukosa usingizi
  30. Huongeza SANA kinga ya mwili
Share:

UFAHAMU WAKATI MZURI WA KUPATA MAWAZO MAPYA NA KUJIONA MWENYEWE

Habari Ndugu:
Katika maisha yako umesha chunguza na ukafahamu ni wakati gani huwa unapata mawazo mapya au ni wakati gani huwa unajisikia furaha utulivu wa akili na hatimaye unapata nguvu mpya ya kusonga mbele kwenye maisha yako? Je, ni wakati ukiwa umelala?, ni wakati ukiwa unaangalia mpira?, ni wakati ukiwa na rafiki yako? Ni wakati ukiwa baa? Au ni wakati gani?
Dunia imejaa kelele nyingi kila mahali, kuna kelele za magari, kuna kelele za watu, kuna kelele za mihemko ya mwili na kuna kelele za wanyama na ndege 

wa angani. Tunayo bahati kubwa sana miili yetu inauwezo wa kuchuja hizo kelele na hatimaye hazikuathiri sana lakini katikati ya kelele hizo  ni vigumu sana kupata wazo jipya na kujiona mwenyewe. Pia katikati ya kelele hizo ni vigumu sana kupata nguvu mpya.
Kuna rafiki yangu mmoja nilimwuliza hivi;  “Ni wakati gani huwa unapata mawazo mapya?” “Akasema kwa kweli mara nyingi sana nikiwa naangalia mpira huwa napata mawazo mapya na siku nyingine nikiwa napiga stori na marafiki zangu huwa napata mawazo mapya”.
Nikamwuliza kwa namna hii “Ni wakati gani huwa unajiona mwenyewe? Akashangaa! kujiona mwenyewe? Mbona kila siku huwa najiona hata sasa najiona au unamaanisha nini? Nikamwambia sina maana nyingine ni hiyo hiyo ni wakati gani huwa unajiona mwenyewe? Akasema hapo sijakuelewa naomba ufafanuzi.


Nikaanza kumweleza; mara nyingi sana sisi binadamu huwa hatujioni sisi mwenyewe lakini huwa tunawaona watu wengine, pale wanapofanya mambo mazuri wakati mwingine huwa wa kwanza kutoa maoni yetu juu ya mafanikio hayo au wanapofanya vibaya huwa vile vile wa kwanza kutoa maoni yetu juu ya kufanya vibaya kwao. Wakati tunatoa maoni yetu juu ya watu wengine macho yetu na akili zetu huwa zinasahau kujiona (kujiangalia) sisi wenyewe. Kwahiyo kujiona wewe mwenyewe (finding yourself) ni kule kujitambua kutoka ndani 

yako sehemu ulipo katika mambo yote, mfano kiuchumi, kiroho, kielimu n.k
Mtu anayejiona yeye mwenyewe anakuwa makini na anakuwa na kiu ya kutaka afike sehemu fulani, hapotezi muda bure kwenye mambo yasiyomsaidia kwenye maisha yake, tena mtu anayejiona yeye mwenyewe sio mwepesi wa kutoa maoni juu ya watu wengine maana kabla hajatoa maoni juu ya watu wengine jicho lake litamwona yeye kwanza. Baada ya maelezo hayo akasema hapo nimekuelewa.
Ninachotaka nikushirikishe ndugu kwenye makala hii ni kwamba  kuna wakati ambapo mtu anaweza kujiona yeye mwenyewe wakati huu anapojiona yeye mwenyewe ndipo anapata mawazo mapya yenye kumjenga. Je, ni wakati gani huo?


Ni wakati wa KUPUNGA. Kupunga ndio nini? Kupunga ni wakati ambapo mtu anaenda sehemu tulivu yenye mandhari nzuri na mara nyingi wakati wa jioni au mchana kwa lengo la kutafakari. Mtu huenda kwenye eneo hilo akiwa peke yake. Kupunga ni namna ya kupata mawazo mapya na kujiona wewe mwenyewe na njia hii ilitumiwa tangu enzi za mababu wa kale na kale. Walikuwa wanatumia njia hii ya kupunga kondeni hasa mara baada ya kazi ngumu. Baadaye katika kizazi chetu watu wameanzisha utaratibu wa kwenda 

kupunga na marafiki zao sehemu za fukwe ya bahari au ziwa.
Lakini kupunga yenye lengo la kupata mawazo mapya na kujiona wewe mwenyewe unatakiwa uwe peke yako ukitafakari jinsi ulivyo, maisha yako yalivyo, mwelekeo wako utakuwaje lakini pia ukifurahia mandhari nzuri ya uso wa dunia na wakati mwingine miziki ya sauti za ndege ikiimba kwa mbali. Wafalme wengi walitumia njia hii ya kupunga ili kupata utulivu wa akili na utulivu wa moyo katika kutawala kwao na  jinsi ya kukabiliana na maadui zao.

Je, wewe huwa unapunga?. Kuna faida nyingi sana za kupunga, mimi baada ya kuzifahamu faida hizo mara nyingi huwa napunga. Utanikuta niko sehemu tulivu yenye mandhari nzuri au wakati mwingine huwa naenda mlimani napanda juu ya mlima halafu naanza kufurahia jinsi dunia ilivyo nzuri, jinsi mimi mwenyewe nilivyo mzuri, si hayo tu bali huwa napata msimamo wa maisha yangu. Toka nikiwa kidato cha kwanza nilianza tabia hii ya kupunga mpaka sasa naendelea, kwa kweli ni furaha kubwa. Naomba nikushirikishe baadhi ya faida unazozipata kwa kupunga.

Kubadili msimamo hasi wa kimawazo.
Kupitia kupunga huwa nabadilika kabisa jinsi ya kufikiri kwangu, wakati mwingine huwa moyoni nimejaa fikira potofu za mahangaiko ya hapa na pale lakini nikienda kupunga nguvu mpya hunijia na  mawazo mapya ya kukabiliana na changamoto za maisha yaninijia.

Kupata furaha na raha ya kuishi duniani.
Ni kweli kabisa kama nilivyokudokeza hapo mwanzo, wafalme wengi na mpaka hivi sasa utakuta wana bustani kubwa na nzuri mara nyingi saa za jioni huenda 

kwenye bustani zao na kufurahia maisha. Mara nyingi mimi nikiwa napunga huwa nafurahi sana kuona mimi ni mzima mwenye afya na huwa nafurahi sana kuona dunia jinsi ilivyo nzuri. Zaidi ya yote huwa nafurahi sana ninapowasikia na kuowaona ndege jinsi wanavyoimba na kufurahi. Nikiwa napungia ufukweni huwa nafurahi sana kuona jinsi bahari au ziwa linavyopendeza na wakati mwingine nikiwaona viumbe vya bahari wanavyofurahia maisha wakiruka ruka kwenye ulimwengu wao.

Kutoa wivu, hasira na kujaa upendo.
Wakati mwingine huwa tunakwazwa na mambo mengi sana katika maisha. Ukiwa na tabia ya kupunga utashangaa hizo sumu zinatoweka na badala ya kuwa na hizo sumu unakuwa na upendo mwingi. Kwanza unajipenda wewe mwenyewe na unajiona ni mwenye bahati. Lakini pia kama utakuwa unapungia eneo lenye ndege au wanyama, viumbe hao watakufundisha jinsi wanavyoishi kwa kupendana wakifurahi siku zote.

Kujiona wewe mwenyewe.
Hili ndilo lengo hasa la makala hii, wakati wa kupunga ni wakati wa kujiona wewe mwenyewe. Ndio maana nakushauri unapopunga kwa lengo la kujiona wewe mwenyewe unatakiwa uwe peke yako. Wakati ukiwa unatafakari tafakari utashangaa utakapojiona wewe mwenyewe jinsi ulivyo mzuri, ulivyo barikiwa, tena utajiona wewe mwenyewe jinsi unavyotakiwa kuongeza juhudi kwenye mambo yako mazuri nk. Unapokuwa kwenye kelele nyingi sio rahisi kujiona wewe mwenyewe wala hutajigundua jinsi ulivyo. Nakushauri kama unanafasi anza tabia hii ya kupunga utashangaa jinsi utakavyojiona wewe mwenyewe.

Unapokuwa unapunga ufanye nini zaidi?
Unapopunga unatakiwa kuwa kwenye eneo lenye utulivu, ni vizuri ukazima simu yako ili ubaki peke yako. Unapopunga jifurahie wewe mwenyewe, pumua kwa nguvu halafu jisikilizie jinsi ilivyo raha kupumua, utashangaa wakati unapumua kwa namna hii utaona kila kitu kinachokuzunguka jinsi kilivyo kizuri, anga litakuwa zuri miali ya mwanga itakuwa inadunda dunda hata hakuna lugha ya kuielezea.

Ushauri wangu.
Mpendwa msomaji wa Top Service Care nakushauri anza kuwa na tabia ya kupunga angalau tenga hata siku moja kwa wiki saa ya jioni mara baada ya kazi nenda kwenye eneo zuri ukapunge. Kunafaida kubwa sana ya kupunga hata Mungu mwenyewe huwa anapunga saa ya jioni kama ilivyoandikwa kwenye 

kitabu cha Mwanzo. Mimi naamini nguvu iliyomo wakati wa kupunga, na nitaendelea siku zote kupunga nipatapo nafasi. Kama hujaanza wala hujawahi kujaribu basi mara umalizapo kusoma makala hii jiwekee ratiba ya kupunga halafu utaniambia jinsi ilivyo raha kupunga. Unaweza kuniandikia kwa email
“Kupunga ni namna ya kupata mawazo mapya na kujiona wewe mwenyewe na njia hii ilitumiwa tangu enzi za mababu wa kale na kale. Walikuwa wanatumia njia hii ya kupunga kondeni hasa mara baada ya kazi ngumu”

Tunakuhamasisha ili ufikie mafanikio yako
Share:

UNAPOIHARIBU NAFSI YAKO

Habari yako ndugu na rafiki yangu;
Ninakukaribisha katika tafakari yetu ya leo, ambapo nimekuwa nikikuletea makala hizi kwa lengo la kukusaidia pale unapokwama ili kwa pamoja tusonge mbele katika maisha yetu na lengo langu kubwa ni ili mimi na wewe tufanikiwe. Masomo haya ninayokuletea haya kusaidii wewe tu wala siandiki ili nikufundishe wewe tu, kati ya watu wanaofaidika zaidi na masomo haya ni mimi mwenyewe yananifundisha mambo mengi sana na yananisaidia mambo mengi mno. Huwa na kaa na kutulia naanza kuzisoma makala hizi nilizoziandika mimi mwenyewe 

halafu najifunza mambo mengi ambayo yananisaidia kila siku kwenye harakati zangu za mafanikio. Kwa sababu mafanikio ni vizuri kumshirikisha  mwenzako ndio maana nakushirikisha wewe ili upate kufaidika na hatimaye ufikie mafanikio yako. Mfano mzuri, mwezi wa tano mwaka huu (2015)  nilipata fursa moja ya kujiunga na rafiki zangu wanne ili tuanzishe ufugaji wa kuku. Nilikuwa natakiwa kuchangia shilingi milioni mbili kwenye mradi huo. Kwa wakati huo 

sikuwa na pesa yoyote wala sikujua nitapata wapi pesa hizo. Wakati natafakari hayo nikakumbuka makala moja niliiandika kipindi cha nyuma kidogo yenye kichwa cha habari; Jinsi Ya Kupata Chochote UnachokitakaHaraka haraka nikakimbilia kuisoma makala hiyo, mara nilipomaliza kuisoma nikapata akili nikaanza kuyatumia mafunzo niliyojifunza humo. Baada ya siku mbili nilipata milioni mbili. Nilishangaa sana ndipo nikaelewa kuwa makala hizi ninazoziandika sio kwa ajili yako tu bali pia kwa ajili yangu.

Mara nyingi sana ninapokumbana na tatizo au changamoto fulani huwa natumia makala zangu kama washauri wangu na zimenisaidia sana siku kwa siku. Hivi karibuni nilikuletea makala nyingine yenye kichwa cha habari; Kukiomba Msamaha Kila Kiungo Cha Mwili Wako Ni Siri YaAjabu Kukutoa Kwenye Tabia Sugu. Wakati naendelea kuyafanyia kazi mafunzo yaliyomo kwenye makala hiyo, nimekuja kugundua kwamba usiporekebisha baadhi ya mwenendo wa maisha yako hutaweza kamwe kujinasua na tabia sugu. Tabia sugu maana yake 

ni mwenendo na matendo ambayo umekuwa ukiyafanya, lakini hupendi uyafanye kwa sababu yanakuharibia maisha yako, tena yanakupotezea muda, kibaya zaidi yanakurudisha nyuma kwenye harakati zako za kuelekea mafanikio makubwa. Pamoja na ubaya wa hiyo tabia sugu kwako, bado huwezi kuiacha au unajaribu kuiacha lakini unajikuta umerudia tena. Mfano wa tabia sugu inaweza kuwa ni uvivu, unajitahidi uache uvivu lakini bado unashindwa kuacha, unajikuta unaendelea kulala au kupiga soga mpaka muda wa kufanya mambo mengine ya maana unaisha halafu unajisemea nitafanya kesho na kesho ikifika yana kuwa ni yale yale tu. Tabia sugu inaweza kuwa ni uvutaji sigara unajitahidi 

lakini bado unashindwa kuacha kuvuta sigara.  Inaweza kuwa ni ulevi, unajitahidi uache kunywa pombe lakini unashangaa  umerudia kunywa pombe na unalewa vile vile, japo unapoteza fedha nyingi  ambazo ungezitumia kwenye shughuli nyingine za maendeleo. Inaweza kuwa ni uzinzi, unajitahidi uache lakini unajikuta huwezi kuacha, unaendelea kujilaumu na kujichukia lakini bado tu unafanya, hata hujui utatokaje. Inaweza kuwa ni kuangalia picha za ngono, unajitahidi uache lakini huwezi, ukibaki peke yako tu chumbani na simu au computa yako tayari unahamasika kuangalia picha za ngono na huwezi kujizuia. Tabia sugu inaweza kuwa ni kutotii ratiba yako uliyojipangia, kila mara unajitahidi uamke saa fulani ufanye kazi hii na hii lakini bado unashindwa kufanya hivyo. Hizo ni baadhi tu ya tabia sugu kwa kuzitaja. Wewe mwenyewe unajua tabia sugu yako ni ipi ambayo imekuwa inakusumbua siku nyingi na huipendi lakini ndo hivyo imekunasa.

Katika makala hii; KukiombaMsamaha Kila Kiungo Cha Mwili Wako Ni Siri Ya Ajabu Kukutoa Kwenye Tabia Sugu (kama hujaisoma naomba uisome itakusaidia), nilielezea mambo makubwa mawili yanayoharibu nafsi ambayo ni uzinzi na maneno. Lakini pia nilielezea uhusiano kati ya mwili, nafsi na wewe (maana wewe sio mwili lakini unaishi ndani ya mwili). Nikasema unapokuwa na mahusiano mabaya kati yako na mwili maana yake anayewaunganisha ili muelewane (translator) ambaye ni nafsi amejeruhiwa au amekufa kabisa. Kufa kwa nafsi maana yake imeshindwa kufanya kazi yake kisawasawa. Sasa ili nafsi yako irejee kwenye hali yake ya kawaida ni lazima kuiponya na njia mojawapo ya kuiponya nafsi ni kwa njia ya kuiomba msamaha. Baadaye nitakupa njia zingine.

Nini Kinakusumbua? Unafikiri Ni Kwa Nini?
Mahangaiko yoyote yanayokupata hasa ya moyoni chanzo chake ni kimoja tu ni kuilisha nafsi chakula kisicho sahihi. Nafsi hula chakula kupitia macho, masikio, maneno (ulimi), ngozi nk. Hivi viungo nilivyovitaja kila kimoja kwa nafasi yake na kwa wakati wake hupeleka chakula kwenye nafsi, kama chakula ni sahihi utaisikia nafsi ikifurahi, lakini kama chakula sio sahihi utaisikia nafsi ikihuzunika na kukosa amani halafu unapata mahangaiko mengi moyoni. Mambo yoyote 

yale yanayoihuzunisha nafsi maana yake yanaijeruhi au yanaiua nafsi yako. Hebu fikiria ni kitu gani ambacho kimekuwa kikikuhuzunisha au kukukosesha amani mara kwa mara?. Hebu fikiria chanzo cha kuhuzunika huko ni nini? Je, ni wewe mwenyewe kwa tabia yako sugu au chanzo chake ni nje kabisa ya wewe?. Kama chanzo cha mahangaiko yako ni nje ya mwili wako mfano umesikia ndugu yako anaugua sana, gafula unapata huzuni hiyo chanzo chake ni nje yako na ni vigumu kuyaepuka mambo hayo na wala sio lengo langu kuyazungumzia hayo kwenye makala hii. Lakini kama chanzo cha huzuni yako ni wewe kutokana na tabia yako, basi fanya mambo haya manne yatakusaidia.

Jambo la kwanza: Acha kuilisha nafsi chakula chenye sumu. Chunga macho yako yasitazame mambo usiyoyapenda vinginevyo nafsi itakula sumu. Chunga maneno unayoyatamka pia kuwa makini na maneno unayoyasikia kama uko kwenye eneo lenye maneno usiyoyapenda ondoka haraka sana. Mfano mwingine, kama unapenda kuangalia miziki ya watu wakicheza uchi hapo unaiua nafsi yako, kwahiyo huwezi kujizuia kufanya uzinzi, kama sio uzinzi basi utapiga punyeto. Kwanini itakuwa hivyo? kwa sababu nafsi inakuwa imejeruhiwa haifanyi kazi yake kawaida. Bila kuiponya nafsi uwe na uhakika hiyo itakuwa tabia sugu kwako na hutaweza kuiacha mpaka umeacha kuilisha nafsi chakula chenye sumu.

Jambo la pili; Fanya juhudi za kujipatanisha wewe na mwili wako. Njia pekee iliyodumu vizazi vingi ya kujipatanisha ni kupitia kuomba msamaha. Iombe msamaha nafsi yako, na kila kiungo cha mwili wako ulichokitumia kufanya uovu. Dhamiria kuacha uovu na tumia njia hii ya kuomba msamaha itakusaidia sana, yaombe msamaha macho yako, ulimi wako, miguu yako, mikono yako na kila kiungo ulichotumia kufanya uovu.

Jambo la tatu: Kaa mbali na marafiki wanaokurudisha nyuma. Usijidanganye kwamba nitakuwa nao tu lakini nitakuwa najiepusha na matendo yako. Kumbuka kuna msemo usemao;  “je, unaweza kuweka kaa la moto kifuani na nguo zako zisiungue?” Au “je, unaweza kukanyaga kaa la moto na nyayo zako zisiungue?”. Kuwa makini na hilo, kumbuka hata maneno unayoyasikia yanaweza kuharibu nafsi yako.

Jambo la nne: Usijaribie kufanya uovu eti kwa kisingizio kwamba sasa nimeshajua niko makini sitafanya. Hapo unajidanganya tu, lazima utafanya kama sio leo utafanya kesho kwa kisingizio hicho hicho cha kujaribia tu.

Usipoyazingatia Hayo Kuna Madhara Yoyote?
Usipoyazingatia hayo hutafanya kile unachokitaka, lazima utafanya usiyoyataka halafu utaendelea kuumia moyoni mwako siku zote. Kama una kazi ya kutumia akili, ufanisi wako kwenye kazi hiyo utakuwa mdogo kwa sababu ya kuhuzunika na kujuta. Ni vema ukayazingatia ikiwa unataka kuishi maisha mazuri yenye furaha na amani na mafanikio.

Ushauri Wa Mwisho Kwenye Swala Hili.
Soma kitabu hiki The mastery of loveKitakusaidia kushinda kila tabia sugu inayokusumbua. Nakutakia utekelezaji mwema na Mungu akusaidie uvuke kwenye mahangaiko hayo.

“Tabia sugu maana yake ni mwenendo na matendo ambayo umekuwa ukiyafanya, lakini hupendi uyafanye kwa sababu yanakuharibia maisha yako, tena yanakupotezea muda, kibaya zaidi yanakurudisha nyuma kwenye harakati zako za kuelekea mafanikio makubwa”

Tunakuhamasisha Ili Ufikie Mafanikio Yako
Share:

UTAMU WA MAISHA HUU HAPA

Furaha niliyonayo, haina tena mfano,
Nacheka napiga mwayo, na kuubusu mkono,
Umeburudika moyo, kwa usingizi wa pono,
Njoo mwaka kesho njoo, nende zangu sekondari.

Ndugu nimeanza kwa kionjo cha shairi hilo nikitaka tujifunze kitu. Shairi hilo nalikumbuka lilikuwa limeandikwa kwenye kitabu cha Jipime Kiswahili,shule ya msingi. Kabla ya shule za kata kuanzishwa, kufaulu kutoka shule ya msingi kwenda sekondari ilikuwa kitu kigumu sana hasa kwa wale waliokuwa wanaishi vijijini. Ilikuwa raha kubwa ikitokea ukafaulu na kuwa miongoni wa wanafunzi wachache walioweza  kwenda sekondari. Sasa, tunajifunza nini kwenye shairi hili?. Kama kichwa cha habari hapo juu ilikuwa inaonekana kwamba ukifaulu kujiunga na masomo ya sekondari, huko sekondari maisha ni matamu sana. Lakini mara nyingi ilikuwa tofauti, ilikuwa ukifika sekondari enzi zile unanyanyaswa halafu unaonekana hufai katika dunia hii. Utamu wa maisha uliokuwa unauwazia unakuwa kinyume chake. Kumbe maisha matamu haikuwa kwenda sekondari.

Naomba nikuletee hadithi tatu kuhusu utamu wa maisha kisha kupitia hadithi hizo tatu tutapata kufahamu maisha matamu ni yapi.

Hadithi ya kwanza: Utamu wa maisha ni kupata watu wengi wanaokuunga mkono au kukushangilia. Kuna mtu mmoja alikuwa mchezaji wa mpira wa miguu, kwa sababu alikuwa anafanya vizuri sana kwenye mchezo huu, watu wengi walikuwa wanamshabikia. Baada ya kuwa mchezaji bora kwa muda mrefu, mtu mmoja akamwuliza hivi utamu wa maisha ni nini? Yule jamaa akajibu haraka haraka akasema "Utamu wa maisha ni pale watu wengi wanapokuunga mkono kwenye kazi zako". Muda sio mrefu yule  jamaa akavujika mguu wakati anacheza mpira, cha kushangaza wale waliokuwa wanamshabikia hawakumshabikia tena. Kibaya zaidi hata kule kumfariji tu hawakuja. Baada ya kuona vile akabadilisha mawazo yake akaanza kusema jamani utamu wa maisha sio kuungwa mkono na watu. Tangu siku hiyo akaanza kuwaambia watu wote hata watoto wake kwamba maisha matamu sio kupata washabiki wengi kwa sababu ipo siku hao watu wanaookuunga mkono watakuacha. Kwahiyo maisha matamu sio kuungwa mkono au kushabikiwa na watu.

Hadithi ya pili: Maisha matamu ni kuoa au kuolewa. Kuna mtu mmoja wanaume, kwa muda mrefu alikuwa akiulizwa maisha matamu ni yapi? Alikuwa anatoa jibu moja tu “ Maisha matamu ni pale unapokuwa na mke wako”. Tena katika mahali pale kulikuwa na mwanamke mmoja naye alikuwa akiulizwa maisha matamu ni yapi?. Alikuwa anatoa jibu moja tu “maisha matamu ni pale unapokuwa na mume wako”. Siku si nyingi wale watu walioana; maisha yakaendelea, miezi kadhaa ikapita.  Kweli walikuwa wanakiri wote kuwa maisha matamu ni kuoa au kuolewa. Mwanaume alikuwa anafanya kazi kiwandani, kiwanda cha kutengeneza vitu vya urembo. Siku moja kuna  muuza sukari alipita kwenye familia ya wanandoa hao akiwa anauza sukari; akamkuta mwanamke yupo, mwanaume kama kawaida alikuwa kazini kwake. Yule muuzaji akampenda yule mwananke na akamtaka kimapenzi na kwamba akifanya nae mapenzi atampa sukari bure. Yule mama akakataa lakini baada ya kumshawishi kwa maneno mengi hatimaye akawaza si mara moja tu halafu mume wangu hatajua. Basi, akamkubalia wakaanza kufanya mapenzi.
Siku hiyo kule kiwandani walikuwa wanazindua saa mpya, mume wa yule mwanamke akasema ngoja nichukue hii nimpelekee mke wangu ili awe wa kwanza kuivaa. Akakimbia mbio kwenda nyumbani, kufumba na kufumbua akamkuta mke wake anafanya mapenzi na yule muuza sukari. Mambo yakageuka akamchukia sana  mke wake na hakutaka tena kuishi naye, japo yule mwanamke aliomba msamaha, mume wake alikataa katu katu. Mwisho wa yote yule mwanamke akasema heri nisingekuwa nimeolewa kumbe maisha matamu sio kuolewa. Baada ya maneno hayo akajinyonga hadi kufa. Baada ya kufa, yule mwanaume alikamatwa na kufungwa jela. Akiwa jela akajisemea afadhali kama nisingekuwa nimeoa. Akaendelea kusema kumbe maisha matamu sio kuoa. Kutokana na hadithi hiyo tunapata kufahamu kuwa kumbe maisha matamu sio kuoa au kuolewa.

Hadithi ya tatu: Maisha matamu ni kuwa na mali nyingi. Kuna watu wawili mmoja alikuwa tajiri na mwingine alikuwa masikini. Siku moja yule masikini akaugua sana. Yule tajiri aliposikia kwamba yule masikini anaumwa akaenda kumsalimia, akamhurumia sana kwa jinsi alivyokuwa anaumwa akawa anawaza; sasa huyu masikini ataponaje! afadhali kama angekuwa na pesa angekuwa ananunua hata matunda. Kwa kumhurumia akawa kila akienda kumsalimia anamwachia shilingi 500/=. Yule tajiri akaendelea hivyo hivyo hatimaye masikini akapona.
Siku si nyingi tajiri naye akaugua sana, akalazwa hospitali.  Yule masikini akawa anaenda kumsalimia , halafu kila akienda kumsalimia anamwachia shilingi 500/=. Pamoja nakwamba yule tajiri alikuwa na kila kitu na matunda ya kila aina, hakuweza kuyala. Baada ya hali kuwa mbaya akaanza kusema “ Jamani maisha matamu sio kuwa na mali nyingi”. Siku moja aliwaita watoto wake akaanza kuwaambia kama nitakufa waambieni watu wote kuwa maisha matamu sio kuwa na mali nyingi. Kweli muda sio mrefu  tajiri akafa akamwacha yule masikini anaishi. Kutokana na hadithi hiyo tunapata kufahamu kwamba maisha matamu sio kuwa na mali nyingi.
  
Kama Ni Hivyo, Maisha Matamu Ni Yapi Basi?
Siri ya maisha ni fumbo kubwa lakini ukikaa na kufikiri vizuri unaweza kupata picha jinsi maisha matamu yalivyo. Tumekuwa kukihangaika usiku na mchana tukitafuta maisha matamu. Mawazo ya watu wengi ni kwamba maisha matamu ni kuwa na mali nyingi, na kwa sababu hiyo watu wamekuwa wakipambana kwa kila namna ili wapate pesa au wawe matajiri, eti wakifikiri kuwa wakiwa matajiri watakuwa na maisha matamu. Lakini ukweli ni kwamba maisha matamu hayaletwi na mali.

Falsafa yangu: Maisha Ni Mchezo
Tangu nianze kuitumia falsafa hii, imenisaidia kuelewa maisha matamu ni kitu gani. Nimetumia muda mwingi kufikiri maana halisi ya maisha, utamu wake na uchungu wake. Baada ya kufikiri namna ile nilipata kufahamu kuwa maisha yote anayoishi mtu hapa duniani ni mchezo (is a game). Unacheza kwa namna mbalimbali mfano, unaweza kucheza mchezo wa kufatuta pesa, unaweza kucheza mchezo wa kusaidia watu wengine, unaweza kucheza mchezo wa mpira wa miguu, unaweza kucheza mchezo wa siasa, unaweza kucheza mchezo wa masumbwi nk.

Chukulia kwa mfano, wanandoa wanapotengeneza mtoto ni mchezo mojawapo kama ilivyo michezo mingine. Mchezo wa ngumi umenisumbua sana kichwani mwangu nilikuwa nawaza hivi inakuwaje mtu achague mchezo wa ngumi! mbona ni mateso makubwa?. Baadaye nimekuja kufahamu kuwa, mchezo huu ni sehemu ya maisha kwahiyo hakuna mchezaji anayecheza mchezo amechukia. Kama utacheza mchezo wowote ukiwa huna furaha unapocheza lazima utashindwa mchezo huo. Kama unafikiri nadanganya waulize wachezaji wanaokimbia mbio ndefu au fupi wote wanacheza kwa furaha kubwa japo kama hujawahi kimbia kama mchezaji;  siku ukikimbia utakiona cha mtema kuni ni mateso makubwa. Lakini kwa mchezaji ni raha kubwa.

Baada ya kuanza kuitumia falsafa hii imekuwa msaada mkubwa sana kwenye maisha yangu. Mfano nikiwa  nalima shambani naweza kulima  toka asubuhi mpaka jioni bila kuchoka kwa sababu silimi kama mkulima nalima kama mchezaji. Nachukulia kulima kama mchezo mmojawapo kati ya michezo mingine. Nikiwa ofisini nachukulia kuwa ofisini kama mchezo, kama ilivyo michezo mingine hata kama atakuja mtu wa kumhudumia nafurahi zaidi kwa sababu nacheza mchezo ninaoupenda.

Chukulia Kwa Mfano Siasa
Siasa ni mchezo kama ilivyo michezo mingine. Ndio maana utawakuta wanasiasa wanabadilishana vyama leo alikuwa chama hiki kesho anahamia chama hiki. Wewe ambaye sio mchezaji utaona kama kitu kigeni kwa sababu wewe sio mchezaji na hujui sheria za mchezo huo. Ni kama vile mchezaji wa Yanga anavyoweza kuhamia Simba na akaendelea kubaki kuwa mchezaji. Kama kwenye timu za mpira wa miguu mchezajia anaweza kuhamia timu nyingine pinzani na akahesabika yuko sahihi, kwanini unashangaa ukiwaona wanasiasa wanahamia vyama vingine?. Siasa ni mchezo kama ilivyo michezo mingine. Kuongoza watu ni mchezo kama ilivyo michezo mingine. Viongozi wote tulionao wanacheza kila mmoja na nafasi yake, kama vile kwenye mchezo wa mpira wa miguu kila mtu anachezea namba yake. Vivyo hivyo viongozi wetu wanacheza kila mtu na namba yake uwanjani ila mchezo ni mmoja tu “Uongozi

Nataka Kuwa Tajiri
Napenda kutafuta pesa, napenda kuwekeza, napenda kuanzisha miradi mingi niwezavyo, nafanya hivyo kwa sababu huo ni aina ya mchezo ninaoupenda kuucheza. Sitafuti pesa kama natafuta maisha natafuta pesa kwa kucheza mchezo wa kutengeneza pesa. Nafurahi zaidi nikiwa nacheza mchezo huu, sipendi kucheza peke yangu napenda kucheza kama timu kwa sababu nafahamu ili nishinde mchezo wowote lazima nishirikiane na watu wengine wanaocheza nami ndio maana nakushirikisha wewe ndugu kwenye mchezo huu. Nakuandikia makala hizi ili zikutie moyo halafu uwe mchezaji mzuri. Nafahamu kwenye mchezo wowote kuna kushinda , kushindwa au kutoka sare. Siku nikipata hasara kwenye miradi yangu nafurahi zaidi kwa sababu ni sehemu ya mchezo, lakini siishii kufurahi tu nachukulia kitu kilichonifanya nipate hasara kama somo. Siumii sana moyoni nipatapo hasara najua ili nishinde mchezo huu lazima nikutane na changamoto hizo ili ziniimarishe. Napenda utajiri, wala sifikirii kuwa tajiri ndio nitakuwa na maisha matamu. Kuwa tajiri kwangu ni fursa mojawapo itakayoniongezea wigo wa kucheza michezo mingi zaidi katika maisha yangu, pia utajiri utanisaidia kuwa na wigo mpana zaidi wa kuwasaidia watu wengine kwenye michezo yao ili nao wazidi kufurahi zaidi.

Mungu Ni Mchezaji Mzuri
Ndiyo, Mungu anapenda sifa, anapenda watu wamwimbie anapenda watu wacheze, ndio maana katika maandiko matakatifu anatushauri tumwimbie na kumchezea, anapenda sana michezo lakini anasema tusicheze bila yeye lasivyo michezo yetu itageuka kuwa taabu badala ya kuwa mchezo.

Ona anavyosema: “Hata vijana watazimia na kuchoka, na wanaume vijana wataanguka; bali wao wamngojeao Mungu watapata nguvu mpya, watapanda juu kwa mbawa kama tai, watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu , wala hawatazimia. Isaya 40:30-31”

“Msifuni kwa matari na kucheza; msifuni kwa zeze na filimbi. Kila mwenye pumzi na amsifu Mungu. Zaburi 150:4-6”

Nimekupa mifano hiyo miwili ya maandiko matakatifu kuonyesha Mungu anapenda watu wake tucheze. Unaweza kutafuta maandiko mengine mengi zaidi kwenye dini yako. Mungu anafurahia kuona dunia inalizunguka jua, mwezi unaizunguka dunia na mambo mengine mengi, yote hayo ni michezo aliyoianzisha yeye ili imfurahishe. Maisha yote ni michezo mbalimbali ambayo kwa pamoja inatengeneza kitu kinachoitwamaisha.


Maisha Matamu Nimepata Jibu Lake
Baada ya kuanza kuitumia falsafa hii, kwamba maisha ni mchezo, imeniongezea zaidi wigo wa kufikiri. Lakini katika yote nimeelewa kuwa maisha matamu ni kuwa hai,kuwa mzima wa afya na kufurahia kucheza pamoja na Mungu. Haijalishi unapesa au huna, maisha ni mchezo. Kama unaona maisha ni mateso au ni magumu ni kwa sababu hupendi kucheza mchezo huo, unataka ufanye nini sasa?

Ushauri Wangu Kwako
Kwa sababu maisha yote ni mchezo, unatakiwa ujifunze tabia za michezo mbalimbali. Anza kujifunza kucheza, na siku zote hakuna mchezo unaocheza huku huupendi, kama utacheza mchezo ukiwa umekasirika au unamawazo lazima utafanya vibaya kwenye mchezo huo. Ukiwa kwenye ndoa, ndoa ni mchezo cheza kama mchezaji, ukiwa masomoni, masomo ni mchezo soma kama mchezaji. Kuna michezo mingine inasheria zimeandikwa kama mpira wa miguu lakini kuna michezo mingine sheria zake hazijaandikwa ni lazima uzitafute kwa kusoma vitabu mbalimbali au kuhudhuria semina. Mchezo wa kutafuta pesa ni miongoni mwa michezo ambayo sheria zake utazipata kwa kusoma vitabu na  kujifunza. Anza kufurahia maisha sasa. Usifikiri kwamba, kazi unayoifanya ni ngumu, kama unafikiri ni ngumu hebu fikiria kuhusu mchezo wa mgumi,  je, ni mchezo rahisi? Kama sio rahisi mbona kuna watu wanapenda kucheza?. Jibu ni rahisi tu maisha yote ni mchezo, cheza kwa furaha huku ukifurahia utamu wa maisha yako ukiwa unacheza.
Lakini kumbuka ili ushinde mchezo wowote lazima utii sheria zake, vinginevyo hutashinda kamwe.

“Tumekuwa kukihangaika usiku na mchana tukitafuta maisha matamu. Mawazo ya watu wengi ni kwamba maisha matamu ni kuwa na mali nyingi, na kwa sababu hiyo watu wamekuwa wakipambana kwa kila namna ili wapate pesa au wawe matajiri, eti wakifikiri kuwa wakiwa matajiri watakuwa na maisha matamu. Lakini ukweli ni kwamba maisha matamu hayaletwi na mali”.

Tunakuhamasisha ili ufikie mafanikio yako

Share:
Top Servicare. Powered by Blogger.

Web Design

Popular Posts

INSTAGRAM FEED

@soratemplates

Blog Archive

About